MKUU wa wilaya ya Rombo mkoani Kilimanjaro, Raymond Mwangala amewataka wakazi wa eneo hilo kuwekeza kwenye elimu kwani mataifa mengi yameendelea kutokana na kuwekeza katika elimu.



Mwangala akizungumza kwenye kikao cha tathmini ya elimu ya sekondari na kugawa zawadi kwa wanafunzi waliofaulu vyema kidato cha nne, shule zilizofaulisha na walimu wao amesema Rombo mpya ya maendeleo imezaliwa hivyo jamii iwekeze kwenye elimu.


Amesema hivi sasa wilaya ya Rombo imezaliwa upya ikilenga kutazamwa kwa mtazamo chanja tofauti na awali ilivyozungumzwai na ndiyo sababu eneo la kwanza la Mamsera itawekwa taa za barabarani hadi Mkuu.


"Tunaiona Rombo mpya ya maendeleo, tuna maprofesa wengi nchi nzima wametokea Rombo, kuna madokta, mapadri hata marehemu Gadna G Habash kumbe kwao ni Tarakea na aliyekuwa mdhibiti na mkaguzi mkuu wa hesabu za serikali (CAG) Ludovick Utouh ametokea Rombo," amesema.


Amesema amelenga kushirikiana na jamii ya Rombo kuwekeza kwenye elimu ili maendeleo yapatikane kwani nchi nyingi zilizoendelea zimewekeza katika elimu.


"Matajiri wengi wa Dar es salaam, Dodoma, Arusha na kwingine wametokea Rombo, tunataka Rombo mpya ya maendeleo, watu waje Rombo kuona utalii wa mtori na ndizi na watu wenye maendeleo," amesema.


Ofisa elimu sekondari wa halmashauri ya wilaya ya Rombo, Silvanus Tairo amesema kikao hicho kitakuwa chachu ya kuongeza ufaulu mzuri kwa wanafunzi kwani wamejipangia mikakati ya kuboresha elimu na kupambana na changamoto zilizopo.


Tairo amewapongeza walimu waliofanikisha wanafunzi 1,700 kupata daraja la kwanza hadi daraja la tatu ambao ndiyo wenye sifa za kuendelea na elimu ya juu na vyuo mbalimbali.


"Lengo ni kufanya tafakuri ya elimu na kuweka mikakati ambayo itatusaidia kufanya vzuri zaidi kwenye mitihani ijayo na pia kuwapa motisha wanafunzi, walimu na shule husika kufanya vyema zaidi," amesema Tairo.


Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Prof Adolf Mkenda ambaye pia ni mbunge wa Rombo, akizungumza kwa njia ya simu, amewapongeza walimu kwa namna wanavyojitahidi kunyanyua kiwango cha elimu kwa kuwafundisha wanafunzi.


"Nawaahidi kuwa tutaendelea kushirikiana pamoja walimu wangu ili sekta hii muhimu iweze kuwanufaisha watoto wetu ambao watakuwa na manufaa kwa Taifa," amesema Prof Mkenda.


Kaimu mkurugenzi mtendaji wa halmashauri ya wilaya ya Rombo, Christina Marwa ameipongeza idara ya elimu sekondari kwa ubunifu huo wa kufanya tathimini na kutoa zawadi kwa ufaulu.


"Tumeona jambo hili ni jema mno hivyo mwakani mjipange upya na kulifanya kwani litakuwa na matokeo chanya kutokana na hamasa hii iliyofanyika kwa walimu na wanafunzi," amesema Marwa.


Mmoja kati ya wanafunzi walipatiwa zawadi kwa ufaulu mzuri Deus Mdee wa shule ya sekondari Kelamfua amesema motisha walizopata zitaongeza ari kwa wanafunzi kusoma zaidi na walimu kufundisha kwa moyo wote.


"Nashukuru kwa zawadi ya madaftari kwani lengo langu ni kuwa daktari na sasa nasubiria kupangiwa shule ili niende na masomo ya kidato cha tano," amesema.

 

Mkutano Maalum wa 53 wa Baraza la Mawaziri la Jumuiya ya Afrika Mashariki umefanyika leo tarehe 25 Aprili 2024 Makao Makuu ya Jumuiya hiyo jijini Arusha.

Mkutano huo, pamoja na masuala mengine umejadili na kupitisha Makadrio ya Bajeti ya Jumuiya ya Afrika Mashariki kwa mwaka wa fedha 2024/2025.

Ujumbe wa Tanzania katika Mkutano huo umeongozwa na Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Mhe. Stephen Byabato (Mb.).

Viongozi wengine walioshiriki mkutano huo ni pamoja na Naibu Waziri Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora Mhe. Ridhiwani Kikwete (Mb.) na Katibu Mkuu Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki anayeshughulikia masuala ya Afrika Mashariki Balozi Stephen Mbundi

Mkutano huo umefanyika kufuatia kukamilika kwa kikao cha ngazi ya Makatibu Wakuu kilichofanyika tarehe 24 Aprili 2024 ambacho kilitanguliwa na kikao cha ngazi ya Wataalam cha tarehe 23 Aprili 2024.







Mkurugenzi wa Tume ya Usuluhishi na Uamuzi (CMA), Mhe. Usekelege Nahshon Mpulla, amewataka wananchi kuhakikisha wanawasilisha migogoro ya kikazi kwa wakati ndani ya Tume badala ya kuzipeleka kwa wakuu wa wilaya na sehemu zisizohusika.

Ametoa wito huo leo Aprili 25,2024 wakati akifanya mahojiano katika ofisi za makao makuu ya Tume jijini Dodoma.

Mkurugenzi amesema pale wananchi wanapokua na changamoto za migogoro ya kikazi na kuipeleka katika ofisi za wakuu wa wilaya na mahali pengine tofauti na Tume ni sababu mojawapo inayopelekea kuchelewa kufungua migogoro ndani ya Tume.

Aidha, Mpulla amesema elimu kuhusu migogoro ya kikazi imesaidia pia kupunguza idadi ya migogoro inayosajiliwa Tume kutokana na idadi ya migogoro kupungua kutoka idadi ya migogoro 17,963 iliyosajiliwa kwa kipindi cha mwaka 2021/2022 hadi kufikia migogoro 11,759 kwa mwaka 2022/2023 na kupungua hadi kufikia idadi ya migogoro 4,579 ambayo ni hadi February 2024.

Ameongeza kuwa, lengo la Tume ni kuhakikisha inaokoa muda kwa kuwasaidia wadaaawa kupata suluhu ya migogoro yao ili kuweza kuokoa muda kwani usuluhishi ndio njia bora zaidi katika utatuzi wa migogoro ya kikazi na kuwasaidia wadaawa kuendelea na shughuli za kimaendeleo.

Vilevile ameipongeza serikali ya awamu ya sita kwa kusaidia Tume kuhakikisha wanafanikisha shughuli mbaalimbali za Tume zilizopelekea kuboresha huduma na kupunguza migogoro ya kikazi.
Akitoa shukrani hizo ameongeza kuwa Tume imepata fedha kwaajili ya kusimika mfumo wa kusajili mashauri na ambao utawezesha watanzania na watu wote wenye changamoto ya migogoro mahala pa kazi kujisajili kokote waliko ikiwa na lengo la kupunguza gharama ya kufuata ofisi za Tume kwaajili ya kufungua migiogoro.

Aidha, Mpulla amesema mfumo mpya wa kusajili mashauri unaoendelea kusimikwa maeneo mbalimbali nchini katika ofisi za Tume, utasaidia pia katika kuhakikisha wadau mbalimbali wenye migogoro ya kikazi kufungua migogoro kwa wakati kwa muda uliolekezwa kisheria kwa lengo la kupunguza changamoto za kuwasilisha madai Tume baada ya muda kupita.

Vilevile amewataka waajiri na waajiriwa kutumia njia ya usuluhishi ili kuweza kuokoa muda na kuendelea na shughuli za uzalishaji mali na maendeleo kwani ndio njia bora katika utatuzi wa migogoro ya kikazi na yenye faida nyingi kulinganisha na njia ya uamuzi.

 


Kamishna msaidizi wa Ardhi mkoa wa Arusha Geofrey Mwamsojo leo, Alhamisi Aprili 25.2024 amemrejeshea kiwanja na kumkabidhi hati mama mjane aliyetambulika kwa jina la Arafa Mohammed mkazi wa...., jijini Arusha ambaye takribani miaka 15 amekuwa akifuatilia haki yake baada ya kudhulumiwa na mtu mmoja aliyemtaja kwa jina la Alex Mtinange naye akiwa ni mkazi wa jijini humo

Akizungumza na wanahabari wakati wa kukabidhi hati hiyo Kamishna Mwamsojo amesema mama huyo ambaye marehemu mume wake alikuwa raia wa kigeni alifikisha malalamiko hayo mbele ya Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya makazi Jerry Silaa alipoendesha kliniki ya ardhi jijini Arusha hivi karibuni ambapo alieleza kuwa marehemu mume wake alijenga nyumba kwenye kiwanja hicho na walikuwa wakiishi wote kama familia lakini baada ya muda mume wake alianza kuugua, na katika harakati za kupigania uhai wake alimpeleka kumuuguza kwenye nchi mbalimbali huku nyumbani akimuacha binti yake

Hata hivyo baada ya mume wake aliyekuwa raia wa... kufariki, mwaka 2012 mama huyo ambaye kiasili ni mzaliwa wa Tanga alifika kwenye nyumba hiyo lakini katika hali isiyokuwa ya kawaida alimkuta mtu tofauti akiishi, na alipofuatilia ndipo alipoelezwa kuwa nyumba hiyo kwa sasa inamilikiwa na Alex Mtinange ambaye inatajwa kuwa alikuwa kwenye mahusiano ya kimapenzi na binti yake

Inaelezwa kuwa awali wawili hao (binti wa mama huyo mjane na mpenzi wake Alex Mtinange) walikuwa wakiishi wote kwenye nyumba hiyo lakini baadaye waliingia kwenye mgogoro uliopelekea binti huyo kukimbilia nchini Kenya na ndipo Mtinange alipotumia nafasi hiyo kwa kushirikiana na Mwenyekiti wa serikali ya mtaa kujimilikisha kinyume cha sheria

Jitihada mbalimbali ambazo zilichukuliwa na mama huyo ili kurejesha nyumba yake ziligonga mwamba, hadi hivi karibuni jambo hilo lilipotua kwenye meza ya Waziri Silaa aliyetoa maelekezo kwa Kamishna msaidizi wa Ardhi mkoa wa Arusha kufuatilia na kuhakikisha mama huyo anapata haki yake, jambo ambalo limefanikiwa, ingawa nyumba iliyokuwa imejengwa ilikuwa imebomolewa na hivyo kubaki kiwanja pekee

Akizungumza baada ya kukabidhiwa hati hiyo mama huyo ametoa shukrani kwa serikali kupitia Waziri Silaa na Kamishna Mwamsojo kwa kumpigania kuhakikisha anapata haki yake, hata hivyo ametoa wito kwa viongozi na watendaji mbalimbali wa serikali nchini kuiga mfano wa viongozi hao wa kuhakikisha mara zote wanasimamia haki za wananchi ambao wengi wao wamekuwa wakizihangaikia kwa muda mrefu bila mafanikio 

Katika hatua nyingine Kamishna msaidizi wa Ardhi mkoa wa Arusha Geofrey Mwamsojo amesema atahakikisha anamaliza migogoro yote ya ardhi iliyoko mkoani humo, na kwamba ndani ya siku 90 alizopewa na Mkuu wa mkoa wa Arusha Paul Makonda kuhakikisha anamaliza migogoro hiyo anaamini atafanikisha, kwa kuwa kinachofanywa na ofisi hiyo kwa sasa si kuzalisha migogoro mipya bali kushughulikia migogoro ya zamani jambo ambalo linaendelea kwa kasi.






 


Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania - TFS umetoa msaada wa kiasi cha shilingi 20,000,000/= kwa ajili ya kusaidia waathirika wa mafuriko Wilaya za Rufiji na Kibiti mkoani Pwani.

Akipokea msaada huo mapema hivi  leo Mei 25, 2024 Mkuu wa Mkoa wa Pwani, Mhe. Abubakar Kunenge ameshukuru TFS kwa kujali wananchi wakati huu wa changamoto ya mafuriko yaliyosababishwa na mvua zinazoendelea.

 "Fedha hizi zitatumika katika kutoa huduma kwa wananchi wanaopitia changamoto ya mafuriko Rufiji na Kibiti na ninaamini hiki mlichofanya kitaenda kutusaidia mbele kuhakikisha mazingira yanatunzwa,” alisema Mhe. Kunenga

Meneja Uhusiano wa TFS Johary Kachwamba akizungumza kwa niaba ya Kamishna wa uhifadhi Prof. Dos Santos Silayo, amesema TFS inatoa pole kwa waathirika wa mafuriko kwa maeneo mbalimbali nchini ikiwa ni pamoja na Rufiji na Kibiti,

"TFS ina misitu yenye hekta 32,902 ndani ya wilaya ya Rufiji, hivyo wana Rufiji ni Wahifadhi wenzetu na tutaendelea kuwashika mkono kipindi hiki cha changamoto ya mafuriko" Johary.

 



Na Mapuli Kitina Misalaba

Ofisi ya mkuu wa Wilaya ya Shinyanga kwa kushirikiana na viongozi mbalimbali, wadau na wananchi leo asubuhi Aprili 25,2024 wamefanya usafi wa mazingira na kupanda miti 650 katika eneo la Hospitali ya Manispaa ya Shinyanga ikiwa ni sehemu ya maadhimisho ya Miaka 60 ya muungano wa Tanganyika na Zanziber.

 Mgeni rasmi katika shughuli ni katibu tawala wa Wilaya ya Shinyanga Bwana Said Kitinga akimwakilisha mkuu wa Wilaya ya Shinyanga.

Pamoja na mambo mengina Bwana Kitinga ameikumbusha jamii kuendelea kupanda miti katika maeneo yao kama sehemu ya kukabiliana na mabadiliko ya tabia nchi.

Pia ametoa wito kwa watanzania kuendelea kushikamana na kushirikiana ili kuendeleza amani na usalama nchini.

Amesema ni vema watanzania kuendelea kushikamana  na kushirikiana katika shughuli mbalimbali za maendeleo ili kuendelea kuimarisha umoja na usalama wa taifa.

Afisa maliasili na mazingira wa Manispaa ya Shinyanga Ezra Manjerenga amesema miche ya miti 650 imependwa leo kama sehemu ya maadhimisho ya miaka 60 ya muungano wa Tanganyika na Zanziber ambapo amesema zoezi hilo ni endelevu.

Kwa upande wake Mganga mfawidhi wa Hospitali ya Manispaa ya Shinyanga Dkt. Pierina Mwaluko ameahidi kuisimamia miti hiyo ili iweze kuleta matokeo chanya.

Baadhi ya wananchi na viongozi mbalimbali ambao wameshiriki shughuli ya upandaji miti wameeleza wataendelea kuunga mkono kampeni ya upandaji miti katika jamii ambapo pia  wameahidi kuendeleza amani na umoja wa  taifa hili.

Ofisi ya mkuu wa Wilaya ya Shinyanga kwa kushirikiana na viongozi mbalimbali, wadau na wananchi imefanya usafi wa mazingira na kupanda miti katika Hospitali ya Manispaa ya Shinyanga ikiwa ni sehemu ya maadhimisho Miaka 60 ya muungano wa Tanganyika na Zanziber.

Kauli mbiu ya maadhimisho Miaka 60 ya muungano wa Tanganyika na Zanziber Mwaka huu inasema “TUMESHIKAMANA, TUMEIMARIKA KWA MAENDELEO YA TAIFA LETU”.

TAZAMA PICHA HAPA CHINI Shughuli ya upandami miti ikiendelea katika eneo la Hospitali ya Manispaa ya Shinyanga leo Aprili 25,2024 ikiwa ni sehemu ya maadhimisho ya Miaka 60 ya muungano wa Tanganyika na Zanziber.